UFUNDIKO KUMALIZA TATIZO LA UTAPIAMLO KONGWA

 

 





Mratibu wa kituo cha lishe cha Ufundiko kilichopo wilayani Kongwa Bwana Rashid Mtalumba amesema kuwa zaidi ya miaka kumi iliyopita kituo chao kiliweza kuhudumia watoto 30 wenye utapiamlo lakini mpaka sasa kutokana na lishe bora na elimu wanayotoa wamefanikiwa kupunguza idadi ya watoto wenye utapiamlo hadi kufikia watoto wanne kufikia Januari 2025.

Akiongea na waandishi wa habari Mtalumba amesema kituo cha lishe cha Ufundiko kinajihusika na utoaji wa lishe bure kwa watoto wenye umri wa miaka mitano wenye utapiamlo na kutoa maziwa (Lactogen 1)kwa watoto wachanga ambao mama zao hufariki baada ya kujifungua, wapo katika Kata 9 na vijiji 25 ndani ya Wilaya ya Kongwa vikiwemo vijiji vya Norini matongoro na mautya.

Aidha amesema Ufundiko wanashirikiana na Serikali katika masuala ya lishe na kutoa msaada kwa watoto wenye utapiamlo uliopitiliza kwa kuwapeleka katika hospitali mbalimbali nchini Tanzania kama vile Benjamin Mkapa, Muhimbili na Mlali kwenye kituo cha mazoezi kwa watoto wenye ulemavu.

Ameeleza kuwa watoto wengi wenye utapiamlo ni wale wanaozaliwa na watoto yaani wasichana wadogo wenye umri chini ya miaka 18 wengi wao baada ya kujifungua huondoka na kukimbilia mijini kufanya kazi za ndani na kuwatelekeza watoto na bibi zao ambapo hujikita na shughuli za shamba badala ya kutunza watoto.

Mtalumba amesema changamoto kubwa  inayojitokeza katika suala la lishe kwa watoto  ni kuwa wanaume au kina baba wengi hawashiriki katika kupata elimu ya lishe pindi inapowafikia vijijini kwa kuendekeza mfuko dume wa kuwa mwanamke ndiye mwenye jukumu la kupeleka watoto kliniki na sio mwanaume.

Mtalumba ameeleza wasiwasi wake kutokana na Mabadiliko ya hali ya hewa kuwa yanaweza kuathiri sana suala la lishe kutokana na uhaba wa mvua kwani hata chakula cha kawaida kinaweza kisipatikane kwa wananchi.

Bw Mtalumba ameshauri Serikali kupitia kwa maafisa ugani kuendelea kutoa elimu kwa wananchi waweze kulima mazao yanayostahimili ukame kama mtama au watumie njia ya kilimo cha umwagiliaji ili kuongeza uzalishaji wa chakula aidha wazazi watoe chakula kwa kuzingatia makundi ya chakula kwa kutumia vyakula vya asili.

Akiongea katika mkutano wa wadau wa Lishe uliofanyika katika ukumbi wa hospitali ya Wilaya ya Kongwa mkuu wa wilaya ya Kongwa Mhe Mayeka Simon Mayeka amewapongeza wadau hao wa lishe wakiwemo ufundiko na Cuamn kwa mchango mkubwa wanaoutoa katika kusaidia Serikali katika masuala ya lishe na kupunguza idadi ya watoto wenye utapiamlo.

Aidha Mayeka amesisitiza wananchi kutunza mazingira na  kuendelea kutunza chakula walichonacho kwani hali ya hewa iliyopo sio nzuri mvua ni ndogo kutokana na mabadiliko ya hali ya hewa yaliyosababishwa na uharibifu wa mazingira uliofanywa na bianadamu.
 
Source: KongwaDc

0/Post a Comment/Comments